Sifa ziwe kwa Yahu. Na Pasaka dhambi zetu ZOTE zinafunikwa na kuoshwa katika damu ya Mwanakondoo wa Mungu. Tunawekwa huru kutoka katika dhambi—ambacho ndicho hasa kilichokuwa kinaonyeshwa na Waisraeli kuachiliwa kutoka Misri. Pia tulinunuliwa kwa gharama, na sasa sisi ni mali ya Kristo na Baba. Hatumilikiwi na mashirika yoyote yaliyoundwa na wanadamu bali ni wa Yehowah (YHVH), Muumba wetu.
SISI SOTE tumetenda dhambi. Baadhi yetu—angalau machoni pa wanadamu—tumefanya dhambi kubwa zaidi kuliko wengine, ingawa dhambi yote inastahili adhabu ile ile ya mwisho: kifo. Ama kifo chetu wenyewe, au kukubali uhai wa Masihi uliotolewa kulipia adhabu yetu. Ninaleta jambo hili kwa sababu watu wengi hupenda kuwakumbuka watu kwa kushindwa kwao. Mungu huwakumbuka watoto Wake kwa kadiri walivyotumia Roho Wake kushinda hata dhambi mbaya zaidi. Je, kweli mnafikiria kwamba tutakapokutana na Rahabu wa Yeriko tutasema, “Oo, wewe ndiye kahaba yule. Wewe ni Rahabu kahaba?” Kweli? Au tutahesabu kuwa ni heshima kukutana na mmoja wa wanawake watano tu waliotajwa kwa jina au kudokezwa katika nasaba ya Kristo? Endeleeni kufuatilia ujumbe wangu kuhusu wanawake katika nasaba ya Masihi—kwa sababu unahusiana kabisa na Pasaka na siku za Mikate Isiyotiwa Chachu.
Huenda ukataka kusoma sehemu iliyobaki ya blogu hii ikiwa wewe ni mmoja wa wale wanaoamini kwamba aina fulani za dhambi na watenda dhambi wako nje kabisa ya ukombozi au mabadiliko. Ikiwa wewe ni mmoja wa wale wanaohisi kwamba aina fulani za watenda dhambi waliotubu hawapaswi kamwe kuwa sehemu ya ushirika wenu wa wenye haki, basi kwa kweli unahitaji blogu hii. Ikiwa unaona aibu kuwa na watu fulani wakihudhuria pamoja na kikundi chako, endelea kusoma, kwa maana unahitaji sana ujumbe huu. Unahitaji blogu hii ikiwa WEWE mwenyewe unahisi kwamba hutawahi kubadilika au kushinda! Unahitaji ujumbe huu ikiwa mara kwa mara unakaa ukitafakari maisha yako ya zamani yaliyovunjika badala ya kuthamini maisha mapya tuliyo nayo katika Yeshua. Unahitaji blogu hii ikiwa wewe ni mmoja wa wale roho wenye huzuni wanaokumbuka dhambi za watu badala ya kufurahia maisha yao yaliyobadilika au yanayobadilika.
Kwa hiyo soma sehemu iliyobaki ya blogu hii na ufurahie muujiza wa Pasaka na siku za Mikate Isiyotiwa Chachu. Yote yanahusu Yehowah kuwaita watu walioandaliwa kwa ajili ya Mfalme wao na walio tayari kuiongoza dunia katika njia ya Ufalme. Inahusu toba na mabadiliko ya kweli—na kwamba kile kinachohesabika ni jinsi tunavyoishia. Furahia sehemu iliyobaki ya blogu…
Lakini hoja kuu ni hii: haijalishi maisha yetu ya zamani yalikuwa vipi—mazuri au mabaya—kile ambacho Yehovah ataangalia ni TUNAVYOISHIA. Ikiwa maisha yetu ya zamani yanatuweka katika kundi la “watenda dhambi wabaya zaidi,” kuanzia sasa wewe na mimi na wengine tunaweza kumruhusu Kristo aliyefufuka aishi katika maisha yetu na kuonyesha ulimwengu kile ambacho Roho Wake anaweza kufanya kubadilisha MTU YOYOTE, hata mbaya kuliko wote. Ulimwengu hupenda kufundisha kwamba haiwezekani kwa baadhi ya watenda dhambi kubadilika KAMWE. Lakini hilo linakanusha nguvu ya Roho Mtakatifu na kumdharau Baba yetu anayetuzaa upya, anayetufanya tupate kuzaliwa mara ya pili, maisha mapya. Haya si kurudia yale ya zamani, bali ni maisha mapya kabisa. HAKUNA lisilowezekana na Mungu. Inawezekana kabisa kwake na kwa Roho Wake kumgeuza mlevi kuwa mtu anayesimama kama mfano bora wa kiasi. Inawezekana sana kwake kubadilisha wazinzi na wale waliotawaliwa na tamaa za ngono. Inawezekana kabisa kwake kuwageuza mashoga na wenye mahusiano ya jinsia zote mbili kuwa watu tofauti kabisa. Ninataja mifano hii yote kwa sababu hizi ndizo aina za watu ambao ulimwengu husema hawatabadilika kamwe—lakini Neno la Mungu linasema vinginevyo. Mimi namwamini Baba kulingana na Neno Lake na naamini kile ANACHOWEZA kufanya, bila kujali watu wa kimwili wanasema nini kuhusu kutowezekana kwa wengine kubadilika.
Hebu tuone Maandiko yanasema nini:
1 Wakorintho 6:9-11
Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, 10 wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi. 11Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu wetu.
Ni lazima TUBADILIKE. Ni lazima tupokee moyo mpya kutoka kwa Mungu. Tunahitaji kumwomba atutakase na afanye upya Roho Wake ndani yetu, kama Daudi alivyoomba katika Zaburi 51. Ni lazima tuache dhambi zetu za zamani, tukianzia na mawazo yetu! Tunahitaji kumtafuta Muumba wetu zaidi na zaidi katika maombi, kwa sababu ni tunapokaa ndani ya Kristo ndipo tunakuwa na tumaini la kuzaa matunda mengi (Yohana 15:4-5).
ISAYA 55:7
Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Yehowah (BWANA), Naye atamrehemu; Na arejee kwa Elohim (Mungu) wetu, Naye atasamehe kabisa.
EZEKIELI 18:21-24, 26-28
21 “Lakini mtu MBAYA akighairi, na kuacha dhambi zake zote alizotenda, na kuzishika amri zangu zote, na kutenda yaliyo halali na haki, hakika ataishi; hatakufa. 22 Dhambi zake zote alizozitenda hazitakumbukwa juu yake hata mojawapo; katika haki yake aliyoitenda ataishi. 23 Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu?” Asema Yehovah (Bwana MUNGU), “si afadhali aghairi na kuiacha njia yake, akaishi?
24 “Bali mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, na kufanya machukizo yote kama yale afanyayo mtu mwovu, je, ataishi? Katika matendo yake yote ya haki aliyoyatenda halitakumbukwa hata mojawapo; Katoka kosa lile alilolikosa, naam, katika dhambi yake aliyoitenda, atakufa.
26 “Mwenye haki atakapoghairi na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, akafa katika uovu huo; katika uovu wake alioutenda atakufa. 27 Tena, mtu mwovu atakapoghairi, na kuacha uovu wake alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki, ataponya roho yake, nayo itakuwa hai. 28 Kwa sababu atafakari, na kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda, hakika ataishi; hatakufa.”
Ndugu zangu katika Kristo, jambo halijaisha mpaka litakapokwisha. Kuna mtu mahali fulani aliyekuwa anahitaji ujumbe huu. Ruhusu Roho wa Mungu akubadilishe. Tubu dhambi zako za zamani, hata kama zilikuwa mbaya kiasi gani. Mungu wetu atasamehe kwa wingi na atakumbuka jinsi ULIVYOISHIA, bila kujali watu wanakuonaje.
Sauli, ambaye mnajua kama Mtume Paulo, alikuwa mtu mwenye jeuri aliyewakamata, kuwafunga gerezani na hata kuwaua Wakristo wa kwanza (Matendo 22:4, 17-20; 1 Timotheo 1:13,15). Ndiyo maana alijiita “mwenye dhambi mkuu.” Lakini leo tunamkumbuka vipi? Si kama mtesi bali kama mhubiri mkuu wa habari njema tuliyo nayo sote katika Masihi. Yeye—labda kuliko mtume mwingine yeyote—alisambaza Neno katika ulimwengu uliokuwa unajulikana wakati huo. Ni jinsi ALIVYOISHIA ndiyo iliyohesabika.
Wazo linguine moja: nimegundua kwamba wale wanaojua kwamba wamesamehewa sana, hupenda sana (Luka 7:47). Mtu maarufu aliwahi kusema hivyo. Wanaonyesha na kuhisi shukrani ya kina zaidi, upendo na mshangao kwa Mwokozi mkuu tuliyenaye katika Yeshua.
Daudi—namkumbuka kama mtu aliyekuwa na moyo unaompendeza Mungu, si kama muuaji wa Uria. Samsoni, namkumbuka kama mtu wa imani kubwa mwishoni mwa maisha yake, si kama “Samsoni na Delila.” Rahabu, namjua kama mwanamke aliyemwamini Mungu wa Israeli na wakati wa Siku za Mikate Isiyotiwa Chachu aliteremsha kamba nyekundu, ishara ya damu ya Masihi aliyokuwa akiitegemea. Hapana, kwangu yeye si “Rahabu kahaba.” Petro, ambaye alimkana Masihi wake mara tatu (na sisi sote TUMEFANYA hivyo), namkumbuka kama mtume mkuu aliyelia kwa uchungu baada ya kumkana rafiki na Bwana wake (Mathayo 26:74-75). Mapokeo yanasema kwamba wakati wa kifo chake alihisi hastahili kusulubiwa kwa namna ile ile kama Bwana wake, hivyo Petro alisulubiwa kichwa chini. Wakati huu hakumkana Bwana wake na alisimama imara hadi mwisho. Paulo—licha ya maisha yake ya zamani—alijua mwishoni mwa maisha yake kwamba taji ya haki na uzima wa milele vilimngojea, kwa maana alijua kwamba katika Kristo alikuwa amepigana vita vizuri na kudumisha mwendo wake. Tafadhali soma 2 Timotheo 4:6-8.
Ndugu zangu, ni lazima tuwape tumaini kila mmoja kwa kumtia moyo mwenzake mara kwa mara. Kwa kuwafanya ndugu zetu katika Kristo wajue kwamba tunawaona kama wapya, kama waliotakaswa, kama waliosamehewa, kama watoto wapya wa Mungu—si kama watenda dhambi wachafu wa zamani waliokuwa hapo awali. Tunapoona ndugu na dada zetu wakiamini katika nguvu ya ukombozi ya damu ya Mwanakondoo ndani yetu—basi SISI pia tunahimizwa kufanya bidii zaidi kumruhusu Yeshua aliyefufuka aishi ndani yetu. Tunahitaji sana kuona kwamba wengine wanaona ukuaji na mabadiliko ndani yetu. Hilo linatia moyo sana. Ni lazima “tuwaone” kila mmoja wa ndugu na dada zetu katika Kristo kama wapya, na tuhamasishane kudumisha mwendo!
Kwa hiyo, haijalishi maisha yetu ya zamani yalikuwa mazuri sana au machafu—kumbukeni kwamba kile kinachohesabika ni jinsi tunavyoishia. Pasaka inatupa fursa hiyo ya kuwa wapya, ya kufanya vitu vyote kuwa vipya katika maisha yetu. Sifa ziwe kwa Mwanakondoo wa Mungu, Mkombozi na Mwokozi wetu.